Advertisement

Breaking

Wednesday, September 14, 2016

Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BOT) Profesa Beno Ndulu Atoa Taarifa Kuhusu Hali Halisi ya Uchumi wa Tanzania


1.0    Hali ya Uchumi wa tanzani


1.1  Ukuaji wa Uchumi


Kwa mujibu wa takwimu kutoka Ofisi ya Takwimu ya Taifa, hali ya ukuaji wa uchumi wa Tanzania imeendelea kuwa ya kuridhisha. Katika robo ya kwanza ya mwaka 2016, ukuaji wa Pato la Taifa unakadiriwa kuongezeka kwa asilimia 5.5 ikilinganishwa na ongezeko la asilimia 5.7 kipindi kama hicho mwaka 2015 (Kielelezo Na. 1).


Kielelezo Na. 1: Mwenendo wa Ukuaji wa Uchumi Robo ya Kwanza ya Mwaka (Asilimia)


Chanzo: NBS, Ukokotoaji - Benki Kuu



Shughuli zilizochangia ukuaji huu wa uchumi kwa kiasi kikubwa ni pamoja na kilimo (asilimia 11.7), biashara (asilimia 10.6), uchukuzi (asilimia 10.1), sekta ya fedha (asilimia 10.1) na mawasiliano (asilimia 10.0). Shughuli za kiuchumi zilizokua kwa kasi ya juu zaidi katika robo ya kwanza ya mwaka 2016 ni sekta ya fedha (asilimia 13.5), mawasiliano (asilimia 13.4), na utawala wa umma (asilimia 10.2) (Kielelezo Na. 2).


Kielelezo Na. 2a: Ukuaji wa Shughuli Mbalimbali za Uchumi Robo ya Kwanza ya Mwaka (Asilimia)







Kielelezo Na. 2b: Mchango wa Shughuli Mbalimbali za Uchumi katika Ukuaji wa Uchumi Robo ya Kwanza ya Mwaka (Asilimia)







1.2 Matazamio ya Ukuaji wa Uchumi Mwaka 2016


Kwa kuangalia viashiria mbalimbali inaonekana kuwa hali ya uchumi wetu itaendelea kuimarika katika mwaka 2016. Kwa mfano:



Uzalishaji wa umeme nchini katika nusu ya kwanza ya mwaka 2016 umeongezeka kwa asilimia 14.5 kufikia kWh milioni 3,454.2 ikilinganishwa na kWh milioni 3,016.7 katika kipindi kama hicho mwaka 2015. Ongezeko hili limetokana kwa kiasi kikubwa na jitihada za serikali katika kutumia nishati ya gesi kwenye uzalishaji umeme kufuatia kukamilika kwa bomba la gesi kutoka Mtwara na Lindi hadi Dar es Salaam pamoja na mtambo wa Kinyerezi I.

 Umeme unaozalishwa kwa kutumia nishati ya gesi umeongezeka kwa asilimia 52.2 (Kielelezo Na. 3). Hali hii itasaidia kuongezeka kwa uzalishaji viwandani pamoja na sekta nyingine zinazotegemea nishati ya umeme, na hivyo kuchangia katika kuongeza kwa pato la Taifa.  Gharama ya umeme itashuka pia.



Kielelezo Na. 3: Mwenendo wa Uzalishaji Umeme Nchini

Januari - Juni



Uzalishaji wa saruji katika robo ya kwanza ya mwaka 2016 umeongezeka kwa asilimia 7 kufikia tani elfu 725.4 ikilinganishwa na tani elfu 680.1 zilizozalishwa katika robo ya kwanza ya mwaka 2015. Hali hii imechangiwa kwa kiasi kikubwa na ongezeko la uzalishaji wa kampuni ya Dangote ambayo ina uwezo wa kuzalisha tani milioni tatu kwa mwaka (Kielelezo Na. 4).  

Ni matarajio yetu kwamba uzalishaji katika kiwanda cha Dangote chenye uwezo wa tani milioni 3 na katika viwanda vingine vya saruji nchini utaongezeka katika kipindi kilichobaki cha mwaka 2016 kwani mahitaji ya nchi bado ni makubwa kuliko uzalishaji ulivyo hivi sasa.  Aidha kuna miradi mikubwa mingi ya hapo baadaye itakayokuwa na mahitaji makubwa ya saruji kama vile mradi wa reli ya kati.



Kielelezo Na. 4: Mwenendo wa Uzalishaji Sarujii

Januari – Machi



Uagizaji wa malighafi za viwandani kutoka nje umeongezeka kwa asilimia 19.4 katika nusu ya kwanza ya mwaka 2016 kufikia Dola za Marekani milioni 520.2 ikilinganishwa na kipindi kama hicho mwaka 2015 (Kielelezo Na. 5)

Hali hii imechangiwa na kuendelea kukua kwa shughuli za uzalishaji viwandani. Ukuaji huu utaendelea kuchangia pato la Taifa kiujumla katika mwaka 2016.



Kielelezo Na. 5: Mwenendo wa Uagizaji Malighafi za Viwandani

Januari – Juni



Mauzo ya bidhaa za viwanda nje ya nchi yameendelea kukua kwa kasi ya kuridhisha. Katika nusu ya kwanza ya mwaka 2016 mauzo ya bidhaa nje ya nchi yalifikia kiasi cha Dola za Marekani milioni 728.5, sawa na ongezeko la asilimia 15.6 ikilinganishwa na kiasi kilichouzwa kipindi kama hicho mwaka 2015 (Kielelezo Na. 6).



Kielelezo Na. 6: Mwenendo wa Uuzaji wa Bidhaa za Viwandani Nje ya Nchi

Januari – Juni




Makusanyo ya kodi katika nusu ya kwanza ya mwaka 2016 yameendelea kuwa bora zaidi ikilinganishwa na nusu ya kwanza ya mwaka 2015, ikiashiria kuimarika kwa usimamizi wa ukusanyaji wa mapato ya serikali na kuendelea kuimarika kwa hali ya

uchumi wa nchi.



Mikopo itolewayo na mabenki ya biashara kwenye sekta binafsi, imeendelea kuongezeka kwa kasi ya kuridhisha katika nusu ya kwanza ya mwaka 2016 kwa Shilingi bilioni 1,167.2, japo ni pungufu ikilinganishwa na ongezeko la Shilingi bilioni 1,577.5 la mwaka 2015. Ongezeko hili linaendana na malengo ya sera ya mwaka 2015/16 ambayo yanajumuisha utulivu wa mfumuko wa bei (Kielelezo Na. 7).



Kielelezo Na. 7: Mwenendo wa Ongezeko la Mikopo kwa Sekta Binafsi

Januari - Juni



Chanzo: Benki kuu



Miradi mikubwa ya viwanda na miundombinu inayoendelea na inayotarijiwa kuanza kazi siku za usoni itachangia katika kuimarisha uchumi. Hii ni pamoja na:

  1. Ujenzi wa reli ya kati kwa kiwango cha  kisasa (Standard gauge)
  2. Ujenzi wa bomba la mafuta la Uganda ambalo litahusu vile vile upanuzi wa bandari  ya Tanga
  3. Ujenzi wa Export Processing Zone ya Kurasini – itakayokuwa mhimili wa biashara kati ya China na Ukanda huu wa Afrika
  4. Mradi wa kuzalisha megawati 240 za umeme wa Kinyerezi II unaoendelea kujengwa.
  5. Miradi ya kupanua viwanja vya ndege nchini kwa mfano- Dodoma, na mingine inayoendelea -katika viwanja vya Dar es Salaam, Mwanza, Mbeya n.k.
  6. Ujenzi wa maghala ya taifa ya kuhifadhi chakula yenye uwezo wa kuhifadhi tani 350 yatakayojengwa kwa msaada wa Serikali ya Hungary katika sehemu mbalimbali nchini hususan katika mikoa inayozalisha mazao ya nafaka kwa wingi.
  7. Kiwanda cha kuzalisha saruji cha Dangote kilichopo Mtwara ambacho kipo mbioni kuzalisha kulingana na uwezo wake (full capacity);
  8. Kiwanda cha kutengeneza marumaru cha Mkuranga, Pwani ambacho ujenzi wake unaendelea
  9. Kiwanda cha kuzalisha mbolea mkoani Lindi - kinajengwa
  10. Kiwanda cha bidhaa za chuma – mkoani Pwani ambacho kiko mbioni kukamilika.


Kwa kuzingatia mwenendo wa viashiria mbalimbali vya shughuli za uchumi, ni dhahiri kwamba hali ya uchumi wa Tanzania ni nzuri na inatoa matumaini makubwa kwamba shughuli halali za kiuchumi zinaendelea kutekelezwa kama ilivyotarajiwa hapo awali hivyo lengo la ukuaji wa pato la Taifa la asilimia 7.2 kwa mwaka 2016 litafanikiwa. 

Hii inachangiwa pia na ukweli kwamba serikali ya awamu ya tano imejipanga katika kuimarisha uchumi endelevu usiokuwa na mianya ya rushwa; usimamizi thabiti wa rasilimali za umma; na ujenzi wa miundombinu bora kwa lengo la kujenga uchumi wa viwanda chini ya Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano.



1.3  Mwenendowa Mfumuko wa bei


Wastani wa mfumuko wa bei katika miezi sita ya kwanza ya mwaka 2016 umeendelea kuwa mzuri ukiendelea kushuka hadi kufikia asilimia 5.5 mwezi Juni 2016 na asilimia 4.9 mwezi Agosti 2016 kutoka asilimia 6.8 mwezi Desemba 2015 (Kielelezo Na. 8). 

Kushuka huku kwa wastani wa mfumuko wa bei kulichangiwa zaidi na bei zisizojumuisha bei za vyakula na nishati (core inflation) zikifuatiwa na zile za nishati na mafuta. Wastani wa mfumuko wa bei usiojumuisha bei za vyakula na nishati (core inflation), ambao ni kiashiria sahihi zaidi cha utekelezaji wa sera ya fedha, umeendelea kubaki katika viwango vya chini (wastani wa asilimia 2.8 katika miezi sita ya mwanzo ya mwaka 2016) kutokana na hatua mbalimbali thabiti za sera ya fedha na bajeti katika kudhibiti ujazi wa fedha na ukwasi katika uchumi.



Mfumuko wa bei unatarajiwa kuendelea kubakia katika viwango vya tarakimu moja katika siku zijazo na kufikia lengo la muda wa kati la asilimia 5. 

Hii ni kutokana na matarajio ya hali nzuri ya hewa itakayochangia kupungua kwa kasi ya kuongezeka kwa bei za vyakula, pamoja na ongezeko dogo la bei ya mafuta nchini inayotokana na mwenendo wa bei ya mafuta katika soko la dunia, na utulivu wa thamani ya Shilingi. 

Pia, mwendelezo wa sera thabiti ya fedha, usimamizi mzuri wa matumizi na mapato ya Serikali, na upatikanaji wa umeme utokanao na gesi ambao utasaidia kupunguza gharama za uzalishaji viwandani vitaendelea kuimarisha utulivu wa mfumuko wa bei. 

Hata hivyo ni muhimu kuzingatia kuwa upungufu wa mavuno ya mazao ya chakula uliojitokeza kwa baadhi ya nchi za ukanda wa kusini mwa Afrika unaweza kusababisha shinikizo la mfumuko wa bei katika siku za usoni.


Kielelezo Na. 8: Mwenendo wa Mfumuko wa Bei (Badiliko la Miezi 12)


Chanzo: Benki kuu


1.4 Utekelezaji wa Sera ya Fedha


Ili kufikia malengo ya serikali ya kuimarisha uchumi na kudumisha utulivu wa mfumuko wa bei, Benki Kuu imeendelea kutekeleza sera ya fedha inayolenga kudhibiti ukwasi ili uendane na mahitaji halisi ya uchumi. Ongezeko la fedha taslimu (reserve money) ambacho ni kipimo cha ukwasi kwenye uchumi limeendelea kubakia ndani ya malengo katika kipindi chote cha miezi sita ya kwanza ya mwaka 2016. 

Katika kipindi hicho ujazi wa fedha taslimu ulikua kwa wastani wa asilimia 11.6; wakati ujazi wa fedha kwa tafsiri pana zaidi (M3) ulikua kwa wastani wa asilimia 14.4, ikiwa ni ndani ya makadirio ya ukuaji usiozidi asilimia 16.0 kwa mwaka 2015/16.

Wakati huohuo sekta ya fedha imeendelea kuchangia ukuaji wa shughuli mbalimbali za kiuchumi kwa kasi nzuri ya kutoa mikopo kwa wakati na kwa kiwango cha kutosha. Mikopo kwa sekta binafsi ilikua kwa wastani wa asilimia 21.3 katika miezi sita ya kwanza ya mwaka 2016, sawa na kiwango kilichopatikana katika kipindi kama hicho mwaka 2015. 

Mikopo mingi kwa sekta binafsi ilielekezwa kwenye shughuli za biashara kwa wastani wa asilimia 19.3 ya jumla ya mikopo yote, shughuli za watu binafsi wastani wa asilimia 19.0, uzalishaji viwandani wastani wa asilimia 10.6, uchukuzi na mawasiliano wastani wa asilimia 7.9, na shughuli za kilimo asilimia 7.8.

Benki Kuu inaendelea kutekeleza sera madhubuti ya fedha kwa kutumia zana mbalimbali za sera ili kuhakikisha kwamba mahitaji ya ukwasi kwa ajili ya shughuli mbalimbali za kiuchumi yanafikiwa bila ya kuchochea mfumuko wa bei.



1.5     Mwenendo wa Thamani ya Shilingi ya Tanzania


Thamani ya Shilingi imeendelea kuwa tulivu katika nusu ya kwanza ya mwaka 2016, kufuatia hatua mbalimbali za sera ya fedha zilizochukuliwa na Benki Kuu katika kusimamia hali ya ukwasi kwenye uchumi pamoja na mwenendo wa uchumi ndani na nje ya nchi. 

Kuimarika kwa sekta ya nje kulikotokana na ongezeko la mauzo ya bidhaa na huduma nje ya nchi na kupungua kwa thamani ya bidhaa zinazoagizwa kutoka nje kumechangia katika utulivu wa thamani ya shilingi. 

Kupungua kwa thamani ya bidhaa kutoka nje kumechangiwa zaidi na kupungua kwa bei ya mafuta katika soko la dunia. Katika kipindi cha miezi sita ya mwanzo ya mwaka 2016 Shilingi imekuwa ikibadilishwa kwa kati shilingi 2,180 hadi 2,190 kwa dola moja ya Marekani (Kielelezo Na. 9).



Kielelezo Na. 9: Mwenendo wa Thamani ya Shilingi



Chanzo:Benki kuu



Hali hii ya utulivu wa thamani ya Shilingi kwenye soko huru la fedha inadhihirisha kuwa sera thabiti za uchumi pamoja na mwenendo mzuri wa urari wa mapato ya fedha za kigeni, ndio jawabu la kulinda thamani ya shilingi dhidi ya fedha za kigeni na sio kudhibiti matumizi ya dola kama ambayo imekuwa ikidaiwa mara kwa mara. 

Nchi zenye udhibiti mkubwa wa fedha za kigeni mfano Afrika Kusini imeshuhudia kuyumba sana kwa thamani ya fedha yake tofauti na shilingi ya Tanzania.

Hivyo nguvu kubwa inapaswa ielekezwe katika kuboresha mazingira ya uwekezaji katika sekta mbalimbali hususan zile zinazoboresha urari wa malipo ya nje kama vile utalii, viwanda, uchimbaji madini, kilimo n.k. Ikumbukwe kuwa uhuru wa kumiliki na kutumia fedha za kigeni nchini Tanzania uliwekwa kama hatua ya kukabiliana na hali iliyokuwepo miaka ya 1980 ya kuadimika sana kwa fedha za kigeni na mchango wa uhuru huo tumeuona katika kuwepo kwa fedha za kigeni za kutosha. 

Nchi zilizojaribu kuondoa uhuru huo, mfano Zambia, zimeshuhudia kutoweka kwa fedha za kigeni kwenda nje. Hivyo ni jukumu la kila mmoja wetu kuhimiza na kuweka mazingira mazuri ya uzalishaji na kuondokana na fikra za kuingilia soko huru kama jawabu la kulinda thamani ya shilingi.


1.6  Mwenendo wa Sekta ya Kibenki


Katika miezi sita ya kwanza ya mwaka 2016, sekta ya kibenki imeendelea kukua ikichangiwa na uanzishwaji wa taasisi mpya za kifedha ikiwemo Benki ya Waalimu Tanzania (Mwalimu Commercial Bank Plc) na Canara Bank (Tanzania) Limited. Takwimu za awali za tathmini ya hali ya mabenki yetu zinaonesha kuwa mabenki yetu ni imara na salama, yakiwa na mitaji na ukwasi wa kutosha. Kufikia mwezi Juni 2016, kulikuwa na jumla ya benki na taasisi za fedha zinazosimamiwa na Benki Kuu zipatazo 65 zenye matawi 739 nchini kote.

Kiwango cha mitaji kikilinganishwa na mali iliyowekezwa (total capital to total risk weighted assets and off-balance sheet exposures) kilikuwa asilimia 17.17 kikilinganishwa na kiwango cha chini kinachotakiwa kisheria cha asilimia 12.0. Hali ya ukwasi ambayo hupimwa kwa kuangalia uwiano kati ya mali inayoweza kubadilishwa kuwa fedha taslimu na amana zinazoweza kuhitajika katika muda mfupi (liquid assets to demand liabilities) ulikuwa asilimia 37.03 ukilinganishwa na uwiano wa chini unaohitajika kisheria wa asilimia 20 (Jedwali Na. 1).

Amana za wateja katika mabenki zilipungua kutoka shilingi trilioni 20.52 mwezi Desemba 2015 kufikia shilingi trilioni 20.24 mwezi June 2016. Miongoni mwa sababu zilizochangia kupungua kwa amana kwenye mabenki ni pamoja na uamuzi wa Serikali kuhamisha sehemu ya fedha za taasisi na mashirika ya umma kutoka mabenki ya biashara kwenda Benki Kuu ya Tanzania. Aidha mikopo (loans and overdafts) iliongezeka kutoka shilingi trilioni 15.28 mwezi Desemba 2015 hadi kufikia shilingi trilioni 15.67 mwezi Juni 2016.

Upatikanaji wa huduma za kifedha kwa wananchi wasiofikiwa na mabenki umeendelea kuongezeka kutokana na ubunifu wa mipango ya utoaji wa huduma za malipo ya rejareja kupitia simu za mikononi, pamoja na huduma za uwakala wa mabenki (agent banking services).


Kiujumla kwa kuangalia viashiria vyote vya msingi hali ya ukwasi wa benki imeendelea kuwa ya kuridhisha. Benki Kuu katika kusimamia majukumu yake ya kisera, imeendelea kutoa mikopo ya muda mfupi kupitia “reverse repos” pamoja na kununua fedha za kigeni zinazotokana na mauzo ya bidhaa nje ya nchi kutoka kwenye benki. Kwa viashiria hivi ni dhahiri kwamba uamuzi wa serikali wa kuagiza fedha zake zote kuwekwa kwenye akaunti maalum Benki Kuu hakujasababisha sekta ya kibenki kutokuwa na ukwasi wa kutosha na kuacha kukopesha kwa sekta binafsi kama inavyofikiriwa na baadhi yetu.



Ni vyema jamii ya Watanzania ikafahamu kwamba akaunti ambazo fedha za mashirika zimehamishiwa Benki Kuu ni akaunti za kukusanya mapato tu. Akaunti za matumizi bado ziko katika benki za biashara ili kuyawezesha mashirika kufanya malipo kupitia akaunti hizo. Hivyo, bado benki za biashara ni kiungo muhimu kati ya mashirika ya umma na watoa huduma kwa mashirika hayo. Pia hali ya utoaji mikopo kama tulivyoona awali ni nzuri na watanzania wanaendelea kuhudumiwa na benki zetu kama inavyotarajiwa.



Jedwali Na. 1: Viashiria vya Uimara wa Sekta ya Fedha







1.7 Sekta ya Nje na Akiba ya Fedha za Kigeni


Katika miezi sita ya kwanza ya mwaka 2016, nakisi ya urari wa biashara ya bidhaa, huduma na uhamisho mali nchi za nje (current account deficit) ilipungua kwa asilimia 61.7 na kufikia nakisi ya dola za Kimarekani milioni 970.4, kutoka nakisi ya dola za Kimarekani milioni 2,532.5 mwaka 2015. Kupungua huko kulitokana zaidi na ongezeko la thamani ya bidhaa za viwandani, mapato yatokanayo na utalii na huduma za usafirishaji nje ya nchi, pamoja na kupungua kwa thamani ya bidhaa zilizoagizwa kutoka nje ya nchi hususan bidhaa za mitaji, na bidhaa za matumizi ya kawaida. 

Katika kipindi cha miezi sita iliyoishia Juni 2016, kikilinganishwa na kipindi kama hicho mwaka uliotangulia, thamani ya bidhaa na huduma zilizouzwa nje ya nchi ziliongezeka kwa asilimia 14.2 na kufikia dola za Kimarekani milioni 4,473.2 wakati thamani ya bidhaa na huduma toka nje zilipungua kwa asilimia 18.3 na kufikia dola za Kimarekani milioni 5,360.7

Hazina ya fedha za kigeni imeendelea kuwa ya kuridhisha na kuendelea kukidhi mahitaji ya fedha za kigeni kwa ajili ya kuagiza bidhaa na huduma nje ya nchi, ikiwa ni pamoja na kuongeza imani kwa wawekezaji katika uchumi wetu; japo kumekuwepo na ucheleweshwaji wa fedha za wahisani na mikopo ya kibiashara kutoka nje ya nchi.

 Hadi mwezi June 2016, akiba ya fedha za kigeni ilifikia dola za Kimarekani milioni 3,870.3 ambazo zinatosheleza kuagiza bidhaa na huduma kutoka nje ya nchi kwa takriban miezi 4. Wakati huo huo, rasilimali za fedha za kigeni za mabenki (gross foreign assets) zilikuwa kiasi cha dola za Kimarekani milioni 835.0

1.8  Deni la Taifa


Deni la Taifa limeendelea kuongezeka na kufikia dola za Kimarekani milioni 20,851 mwishoni mwa mwezi Juni 2016, kutoka dola za Kimarekani milioni 19,861 mwezi Desemba 2015. Deni la nje liliongezeka kwa asilimia 2.6 na kufikia dola za Kimarekani milioni 16,281 mwezi Juni 2016 (sawa na asilimia 77.8 ya deni la taifa), kutoka dola za Kimarekani milioni 15,864 mwezi Desemba 2015. Hii ilitokana na kuongezeka kwa mikopo mipya pamoja na malimbikizo ya malipo ya madeni. 

Katika deni hilo la nje, asilimia 83.4 ni deni la Serikali na taasisi za umma. Pamoja na ongezeko hilo, takwimu zinaonyesha kuwa deni letu bado ni stahimilivu. Kwa mfano, deni la nje kwa thamani ya sasa (Net Present Value) ni karibu ya asilimia 20 ya Pato la Taifa, ikilinganishwa na ukomo wa asilimia 50 ya Pato la Taifa (Sept-15 DSA). Hii inaonyesha kuwa bado kuna nafasi kubwa ya kukopa bila kuhatarisha ustahimilivu wa deni letu.

Deni la ndani liliongezeka kufikia shilingi bilioni 10,038.4 mwishoni mwa mwezi Juni 2016 kutoka shilingi bilioni 8,597.0 mwezi Desemba 2015.

 Ongezeko hilo lilitokana na Serikali kukopa kupitia dhamana na hati fungani ajili ya kugharamia bajeti ya Serikali kwa mwaka 2015/16, ikichangiwa pia na kupungua kwa misaada na mikopo kutoka nje.

Jedwali Na 2 linaonyesha vyanzo vya fedha za Serikali na matumizi yake katika kipindi cha miezi 6 kuanzia Januari hadi Juni 2016. Kama inavyoonekana jumla ya mapato ya ndani ilikuwa shilingi bilioni 7,267 wakati matumizi ya kawaida (ukiondoa riba) yalikuwa shilingi bilioni 6,488, hivyo mapato yalitosha kulipia matumizi ya kawaida ya Serikali. Hii ni kuonyesha kwamba madeni ya nje na ndani yalitumika kwa ajili ya miradi ya maendeleo pamoja na kurejesha madeni yaliyopita.



Jedwali Na. 2: Vyanzo vya Fedha vya Serikali na Matumizi Yake (Shilingi bilioni)
































































































No comments:

Post a Comment

Sponsor