Advertisement

Breaking

Monday, October 10, 2016

Lipumba Afungua Akaunti Mpya ya Ruzuku CUF.......Benki ya NMB Yalaumiwa kwa Kuvujisha Siri

Siri kwamba Profesa Ibrahim Lipumba amefungua akaunti mpya yenye jina la chama cha Wananchi CUF imefichuka. Wanaolaumiwa kutokana na kufichuka kwa siri hiyo ni watumishi wa benki ya NMB tawi la Ilala.

Prof. Lipumba ni Mwenyekiti wa CUF, anayetambuliwa na Ofisi ya Msajili wa Vyama Vya Siasa huku chama chake kikiwa tayari kimemfukuza uanachama.

Abdul Kambaya, Mkurugenzi wa Habari na Mawasiliano ya Umma anayetambulika na Msajili wa Vyama Vya Siasa pia huku Baraza Kuu la Uongozi la CUF likiwa limemsimamisha uanachama, amenukuliwa na gazeti la Tanzania Daima, akilaani kitendo cha benki ya NMB kuvujisha taarifa za akaunti mpya ya Prof. Lipumba.

“Aulizwe Meneja wa NMB Ilala, kutoa siri za wateja, hayo ndiyo maadili ya kazi yake? Uko wapi usiri kati ya mteja na benki?” alihoji Kambaya.

Hata hivyo, alipotafutwa Kambaya  ili kufafanua uanzishwaji wa akaunti hiyo, matumizi yake na kama yamezingatia matakwa ya Katiba ya CUF na Sheria ya Vyama Vya Siasa, hakuwa tayari kufafanua akidai kuwa si wakati muafaka.

“Tutaeleza mambo hayo kwa wakati muafaka, kama kuna jambo tunakuwa accused (tunatuhumiwa), iulizeni ofisi ya msajili au benki husika, wao wana taarifa kamili,” alisema.

Ofisi ya Msajili wa Vyama Vya Siasa kupitia Sisty Nyahoza imenukuliwa na vyombo mbalimbali vya habari ikikiri kumtambulisha Prof. Lipumba kwa benki ya NMB ili aweze kufungua akaunti hiyo, hata hivyo amedai kuwa ofisi ya msajili haijui matumizi ya akaunti hiyo.

Taarifa za kufunguliwa kwa akaunti mpya yenye jina la CUF kwa malengo yanayodaiwa ni kuchukua ruzuku za chama hicho zilianza kusambaa katika mitandao ya kijamii Alhamis ya tarehe 06 Septemba mwaka huu.

Uongozi wa CUF taifa kupitia kwa Mbarara Maharagande, Naibu Mkurugezi wa Uenezi na Mawasiliano ya Umma umesema kuwa, utatoa taarifa rasmi juu ya suala hilo  leo Jumatatu, tarehe 10 Oktoba.

No comments:

Post a Comment

Sponsor