Advertisement

Breaking

Thursday, November 3, 2016

Taarifa Kwa Umma Kutoka Jeshi La Polisi Makao Makuu.


Jeshi la Polisi nchini, katika kuhakikisha usalama wa raia na mali zao unaimarika, limeendelea na operesheni za kukamata wahalifu wa makosa mbalimbali yakiwemo makosa ya usalama barabarani katika mikoa yote ili kudhibiti vitendo vya uhalifu na wahalifu. 

Katika operesheni hizo, Jeshi la Polisi limefanikiwa kukamata silaha na katika baadhi ya mikoa, wananchi wameweza kusalimisha silaha kwa hiari katika vituo vya Polisi.

Operesheni hizi ni endelevu, na ili tuweze kufanikiwa zaidi katika kudhibiti uhalifu na wahalifu hususani katika kipindi hiki tunapoelekea mwisho wa mwaka, wananchi wanatakiwa kuwa makini na kutoa taarifa za uhalifu na wahalifu haraka kwa kutumia namba za bure 111 na 112 pindi wanapowatilia shaka watu wasiowajua katika maeneo yao ili hatua za haraka ziweze kuchukuliwa.

Kwa wamiliki wa maduka makubwa, hoteli na maduka ya kufanyia miamala ya fedha kwa njia ya simu waangalie namna ya kuweka vifaa maalumu vyenye uwezo wa kurekodi mienendo ya watu wanaoingia na kutoka ama kufuata huduma katika maeneo yao ya biashara.

Pia, wananchi katika makazi yao waimarishe ulinzi kwa kutumia mpango wa ulinzi jirani kwa kuhakikisha wanakuwa na utaratibu wa kubadilishana taarifa za hali ya usalama ili kuhakikisha mitaa yao inakuwa salama wakati wote.

Aidha, Jeshi la Polisi nchini linawataka madereva wa vyombo vya moto kuheshimu na kutii sheria za usalama barabarani ili kuepusha ajali na kuokoa maisha ya abiria na watumiaji wengine wa barabara. 

Jeshi la polisi nchini, litaendelea kutekeleza majukumu yake kwa mujibu wa sheria, bila woga ama upendeleo katika kuhakikisha usalama wa raia na mali zao unaimarika.

Imetolewa na:
Advera John Bulimba - Kamishina Msaidizi wa Polisi (ACP)
Msemaji wa Jeshi la Polisi,
Makao Makuu ya Polisi.

No comments:

Post a Comment

Sponsor