Advertisement

Breaking

Tuesday, October 4, 2016

Profesa Lipumba Apata Pigo........Baraza la Wadhamini CUF Lagoma Kumtambua, Lapanga Kufunga Jengo la Chama



TAMKO LA BODI YA WADHAMINI YA THE CIVIC UNITED FRONT (CUF – CHAMA CHA WANANCHI) KUFUATIA KIKAO CHAKE KILICHOFANYIKA JANA, TAREHE 2 OKTOBA, 2016


Kwa kuzingatia hali iliojitokeza katika chama chetu cha THE CIVIC UNITED FRONT (CUF – Chama Cha Wananchi) kufuatia hatua ya makusudi ya Msajili wa Vyama vya Siasa nchini, Jaji Francis Mutungi, kutupandikizia vurugu na fujo kwa kujipa mamlaka asiyokuwa nayo ya kutuamulia nani awe Mwenyekiti wa Chama, hatua ambayo imesababisha mtu anayeitwa Ibrahim Haruna Lipumba na genge lake tarehe 24 Septemba, 2016 kuvamia na kuhodhi jengo la Ofisi Kuu ya Chama iliyopo Buguruni, Dar es Salaam, Bodi ya Wadhamini ya Chama iliona kuna haja ya kukutana na kuchukua hatua za kukabiliana na matukio hayo.


Bodi ya Wadhamini ya The Civic United Front (CUF – Chama Cha Wananchi) imefanya kikao chake, tarehe 2 Oktoba, 2016 katika Makao Makuu ya Chama, mjini Zanzibar chini ya Mwenyekiti wake, Mhe. Abdallah Said Khatau.


Tumefanya hivyo kwa kutambua wajibu wetu kwa mujibu wa Sheria ya Vyama vya Siasa, Sura 258 ya Sheria za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (Political Parties Act, Cap 258) na Katiba ya CUF ya 1992 (Toleo la 2014).


Ni vyema ieleweke kwamba kwa mujibu wa Sheria ya Vyama vya Siasa, kila chama cha siasa chenye usajili wa kudumu kinapaswa kuunda Bodi ya Wadhamini ambayo ndiyo inayokuwa mmiliki na msimamizi wa mali zote za chama cha siasa husika. Kifungu cha 21 cha Sheria ya Vyama vya Siasa kinalieleza hilo kama ifuatavyo:


“21. —(1) Every political party which has obtained a certificate of full registration shall appoint a board of trustees to manage the properties and any business or investment of the party.


(2) Every board of trustees shall be duly incorporated under the Trustees Incorporation Act and every party shall, not later than sixty days from the date of full registration, submit to the Registrar—
a) the names and addresses of the members of ther board of trustees; and
b) a copy of the certificate of incorporation.”


CUF kilitimiza masharti hayo ya kisheria kwa kuunda Bodi ya Wadhamini, na Katiba ya Chama ya 1992 (Toleo la 2014), Ibara ya 98 ikafafanua zaidi namna inavyopatikana, pamoja na nguvu na uwezo wake kichama, kama ifuatavyo:


“98._ (1) Kutakuwa na Bodi ya Wadhamini ya Chama itakayoteuliwa na Baraza Kuu la Uongozi la Taifa kwa mujibu wa sheria za nchi kwa kipindi cha miaka mitano (5) na mjumbe anaweza kuteuliwa tena baada ya muda wake kumalizika.


(2) Bodi itakuwa na wajumbe wasiozidi tisa (9), watano (5) kutoka Bara angalau wawili (2) wakiwa ni wanawake na wanne (4) kutoka Zanzibar angalau mmoja (1) akiwa ni mwanamke ambao watateuliwa kwa masharti yanayohitajika ya Sheria ya Bodi ya Wadhamini na utaratibu uliowekwa na Baraza Kuu la Uongozi la Taifa.


(3) Bodi ya Wadhamini itakuwa ndiyo mdhamini pekee wa fedha na mali za Chama pamoja na madeni na itafanya shughuli zake kwa mujibu wa sheria na taratibu zilizowekwa na sheria ya nchi inayohusu Wadhamini.
ads



(4) Bodi inaweza kushitaki au kushitakiwa kwa niaba ya Chama.


(5) Bodi itawajibika kwa Baraza Kuu la Uongozi la Taifa la Chama ambalo linaweza kuweka utaratibu unaofaa wa kuendesha shughuli za Bodi hiyo, na itafanya vikao vyake angalau mara mbili kwa mwaka.


(6) Mwenyekiti na Naibu Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini watachaguliwa na Wajumbe wa Bodi kutoka miongoni mwao, kwa sharti kwamba Mwenyekiti akitoka upande mmoja wa Jamhuri ya Muungano, Naibu Mwenyekiti atatoka upande mwengine wa Jamhuri ya Muungano.”


MAAMUZI YA BODI YA WADHAMINI:
Kufuatana na uwezo wake uliotajwa hapo juu na kwa kuzingatia nafasi yake kama mdhamini pekee wa fedha na mali za Chama (rejea Ibara ya 98(3) iliyotajwa hapo juu, Bodi ya Wadhamini imefikia maamuzi yafuatayo:


1. Imepuuza wito wa mtu anayeitwa Ibrahim Haruna Lipumba alioutangaza jana kwamba eti amemtaka mtu mwengine anayeitwa Thomas Malima kuitisha kikao cha Bodi ya Wadhamini. Lipumba kwa sasa si Mwenyekiti tena wa CUF na pia si mwanachama wa CUF baada ya kufukuzwa uanachama na Baraza Kuu la Uongozi la Taifa.


2. Itaendelea kuwajibika kwa Baraza Kuu la Uongozi la Taifa la Chama kama inavyotakiwa na Ibara ya 98(5) ambalo ndilo linaloiteua Bodi na litaheshimu maamuzi yote ya Baraza Kuu la Uongozi la Taifa likiwa ndiyo chombo chenye dhamana ya kusimamia uongozi na uendeshaji wa Chama.


3. Itachukua hatua za kisheria chini ya uwezo wake iliopewa na Ibara ya 98(3) na 98(4) kurejesha chini ya dhamana yake mali zote za Chama zilizovamiwa, kuporwa na kuhodhiwa na Ibrahim Lipumba na genge lake ikiwemo jengo la Ofisi Kuu ya Chama iliopo Buguruni, Dar es Salaam.


4. Itachukua hatua za kisheria chini ya uwezo wake iliopewa na Ibara ya 98(4) dhidi ya Ibrahim Lipumba kumtaka alipe gharama na hasara zote alizozisababisha kwa kuvamia Mkutano Mkuu Maalum wa Taifa wa Chama, tarehe 21 Agosti, 2016 katika Ukumbi wa Blue Pearl, Ubungo Plaza na genge lake kufanya vurugu, ghasia na uharibifu wa mali za hoteli na hatimaye kuvuruga Mkutano Mkuu jambo lililosababisha hasara ya takriban Sh. 600 milioni; na kisha kuvamia Ofisi Kuu ya Chama, Buguruni, Dar es Salaam, tarehe 24 Septemba, 2016 ambapo alisababisha hasara ya takriban Sh. 50 milioni.


5. Itachukua hatua za kisheria chini ya uwezo wake iliopewa na Ibara ya 98(4) kwa kumshtaki Msajili wa Vyama vya Siasa kwa kuingilia maamuzi halali ya vikao halali vya Chama na kulazimisha kukichagulia Chama chetu Mwenyekiti kinyume na onyo lililowahi kutolewa na Mahakama Kuu dhidi ya Ofisi yake kutokuwa na mamlaka ya aina hiyo.


6. Inawahakikishia wanachama wote wa CUF wa Tanzania Bara na Zanzibar kwamba Bodi yao ya Wadhamini iko makini na itasimama pamoja nao kulinda mali zote za Chama.


7. Inaionya Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa iwache kuingilia mambo ya ndani ya uongozi na uendeshaji wa Chama cha CUF.


HAKI SAWA KWA WOTE


Abdallah Said Khatau
MWENYEKITI WA BODI


Joran Lwehabura Bashange
KATIBU WA BODI

No comments:

Post a Comment

Sponsor